Monday, January 25, 2016

Habari Kubwa 3 Za Leo Kwa Mujibu Wa Mtandao .

1. Jipu Latumbuliwa NIDA..
Hii ni habari inayopewa nafasi ya kwanza kwa uzito na mtandao waMjengwablog.com.
Mimi kama mwandishi wa makala nilipata kuliandikia hili la NIDA kwenye safu yangu ya gazetini Raia Mwema mwezi Agosti, 2011. Niliandika haya kwa kichwa cha makala kinachosemeka hapo chini;
' Mradi wa vitambulisho ni kioja kingine!'
"NI Mwanafalsafa yule wa Kiyunani, Ptolemy aliyepata kuandika; ”Ex Africa simper aliquid novi". Maana yake: "Kila kukicha kitazuka kioja kingine Afrika."
Katikati ya dhahma hii ya kiuchumi tuna mfano wa vipaumbele vya Serikali vinavyotia hasira. Mojawapo ni huu unaoitwa Mradi wa Vitambulisho vya Kitaifa. Mchakato wake umeanza tangu mwaka 2007. Ni baada ya Baraza la Mawaziri kuubariki Februari 2 mwaka huo. Mwakani mchakato huu utatimiza miaka mitano. Unagharimu shilingi bilioni 222. Hiki ni kioja kingine!
Maana, mpaka mradi huu uje ukamilike, basi, yumkini kuna ambao watakuwa wameusikia mradi na kufa hata bila kuvikamata vitambulisho vyenyewe. Na pia tujiulize; katika hali yetu ya sasa, mradi wa vitambulisho vya kitaifa una maana gani?
Na hivi hakuna mawaziri wetu wenye uthubutu wa kufungua vinywa vyao kwenye kikao cha Baraza la Mawaziri na kutamka; ”Mh. Rais, tunashauri Mradi wa Vitambulisho Vya Taifa usitishwe na kuwekwa kando mara moja. Si kipaumbele chetu kwa sasa. Ni anasa ya baadae. Tuchote fedha zilizobaki kwenye mradi huo tuziingize katika dharura ya kupunguza hali mbaya ya umeme tuliyo nayo nchini kwa sasa.”
Ndio, Mawaziri wetu ndio wenye kuunda Serikali na wana nafasi ya kuwapa ahueni Watanzania kwa kuwapunguzia mizigo ya matumizi yasiyo ya lazima kwa sasa kama haya ya kugharamia mradi wa Vitambulisho vya Taifa." Mwisho wa kunuu nilichoandika 2011.
Itakapofika Februari 2 mwaka huu, itakuwa imetimu miaka minane tangu Baraza la Mawaziri la Serikali ya Awamu ya Nne libariki mradi huu.
Tumepokea kwa furaha sana hatua hii ya Rais kutumbua jipu hili la NIDA. Swali linabaki , je, katika hali halisi ya sasa, tuna haja ya kutumia mabilioni ya shilingi kugharamia mradi uliokwisha? Kwanini visitumike vitambulisho vya mpiga kura? Au hati za kusafiria. Mradi wa Vitambulisho vya kitaifa umegeuzwa ' ng'ombe wa maziwa'. Wanyonge walio wengi ndio ng'ombe wanaokamuliwa. Mradi huu ni anasa inayopaswa kusubiri.
2. Simbachawene amng'oa Mkurugenzi wa Manispaa...
Ni habari kutoka Dodoma. Ni hatua sahihi, kama Mkurugenzi ameshindwa kuwasimamia walio chini yake hapaswi kubaki kwenye nafasi hiyo. Ni habari inayopewa nafasi ya pili na mtandao wa Mjengwablog.com
3. Serikali ' yajitoa' mgogoro wa Zanzibar
Hii nayo ni habari kubwa inayopewa nafasi ya tatu na mtandao huu. Waziri wa Fedha Dr. Mpango kaweka wazi hilo jana Bungeni Dodoma. Kwamba wenye jukumu la kuitafuta suluhu ya Zanzibar ni Wazanzibar wenyewe.

No comments:

Post a Comment